Monday 8 April 2013

ZANZIBAR YATUNGA SHERIA KUPINGA NDOA YA JINSIA MOJA

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar, tayari imeshatunga sheria 
ya kukataza ndoa za jinsia moja na kuendelea kuitumia sheria ya adhabu ili kushughulikia masuala yote ya aina hiyo.

Waziri wa Katiba na Sheria, B. Abubakar Khamis Bakar, aliyasema hayo kwenye Kikao cha Baraza la Wawakilishi Zanzibar wakati akijibu swali la Mwakilishi wa Jimbo la Wawi, Bw. Saleh Nassor Juma kutoka Chama cha Wananchi (CUF).

Katika swali lake, Bw. Juma alitaka kujua ni lini Serikali itatunga sheria ya kukataza ndoa hizo na kuweka adhabu kali kwa watu ambao watabainika kufanya vitendo hivyo.

Alisema ndoa za jinsia moja ni kinyume na utamaduni Zanzibar ambapo sheria hiyo imeweka adhabu ya kifungo cha miaka saba.

“Katika sheria hii inahusu makosa mengi yakiwemo ya ubakaji, zinaa, usagaji na umalaya ambayo yote yana adhabu ya kifungo
cha maisha au miaka isiyopungua 30 gerezani,” alisema.

Alisema sura ya 13 ya Sheria za Zanzibar, chini ya kifungu cha 157, inakataza aina zote za uhusiano wa jinsia moja iwe kwa kuoana au  namna yoyote hata kusheherekea uhusiano huo.

Aliongeza kuwa, hakubaliani na kauli ya mwakilishi huyo kuwa vitendo hivyo vimeshamiri Zanzibar bali vipo.

“Ni kweli Mheshimiwa Spika, silka na utamaduni na tabia za Wazanzibari, hauruhusu kufanya mapenzi ya jinsia moja lakini sikubaliani na mwakilishi kama vitendo hivi Zanzibar 
vimeshamiri hapa kwetu,” alisema.

No comments:

Post a Comment