Sunday 7 April 2013

WAZANZIBAR WAMKUMBUKA KARUME KWA HITMA





 Zanzibar. Viongozi mbalimbali nchini, jana walishiriki katika hitima na kumwombea dua Rais wa Kwanza wa Zanzibar, Hayati Abeid Amani Karume aliyeuawa kwa kupigwa risasi Aprili 7 mwaka 1972.
Shughuli hiyo iliyofuatiwa na kuweka maua katika kaburi la marehemu Karume, iliongozwa na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein.
Mambo hayo yalifanyika katika jengo la Ofisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kisiwandui mjini Zanzibar jana asubuhi na kuhudhuriwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete.
Viongozi wengine waliohudhuria hitima hiyo ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Dk Gharib Mohammed Bilali, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharrif Hamad, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd na viongozi wastaafu akiwemo aliyekuwa Rais wa pili wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi.
Mbali na kusoma Kurani Tukufu iliyofuatiwa na hitma pia yaliwekwa mashada ya maua katika kaburi la marehemu Karume aliyeuawa akiwa katika ofisi hiyo.
Baadhi ya walioweka mashada ya maua ni Rais wa Zanzibar, Rais wa Muungano, mkuu wa mabalozi aliyepo Zanzibar. Hali kadhalika mjukuu wa marehemu Karume.
Marehemu Karume aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar baada ya Mapinduzi ya Januari 12 mwaka 1964 aliuawa akiwa ametawala kwa miaka minane.     

No comments:

Post a Comment