Wednesday 30 October 2013

SHEIKHE MTANZANIA ATAFUTWA KENYA !!!

POLISI mjini Mombasa, wanamtafuta raia wa Tanzania, Sheikh Ramadhan Juma, kwa tuhuma za kuhubiri chuki na uchochezi wa kidini katika Msikiti wa Masjid Mussa, uliopo Mombasa, nchini Kenya. Pamoja na Sheikh Juma, pia polisi inawatafuta raia watatu wa Kenya, ambao ni washirika wa Sheikh Juma.

Sheikh Juma anatambuliwa kuwa ni kiongozi mwenye itikadi kali za kidini na anadaiwa kutoroka baada ya kuibuka kwa purukushani zilizotokea wakati polisi walipovamia Msikiti wa Masjid Mussa, Alhamisi wiki iliyopita.

Hatua hiyo ya polisi kuuvamia msikiti huo ilikuja baada ya kutokea machafuko ya kidini katika baadhi ya maeneo ya mji wa Mombasa.

Akizungumza kwa njia ya simu na RAI Jumatano jana kutoka Mombasa, Balozi Mdogo wa Tanzania mjini humo, Yahya Jecha, alisema kuwa Sheikh Juma anatafutwa na polisi kwa tuhuma za kuhamasisha waumini wa dini ya Kiislamu wa Mombasa kufanya uasi dhidi ya serikali na polisi wa Kenya.

Inaelezwa kuwa mahubiri ya Sheikh Juma yamekuja baada ya mwanzoni mwa mwezi huu kufanyika mauaji ya viongozi wawili wa Msikiti wa Masjid Mussa, ambao ni Sheikh Abou Rogo na Sheikh Ibrahim Omar.

Akizungumzia hilo, Balozi Jecha alisema kuwa polisi wa Mombasa wana wasiwasi Sheikh Juma ametoroka pamoja na waumini wengine wa Mombasa na kurudi Tanzania.

Kwa mujibu wa maelezo ya Balozi, mahubiri aliyoyatoa Sheikh Juma, yaliwahamasisha Waislamu kutorudi nyuma baada ya vifo vya viongozi wao kwa kuwataka kuingia mitaani.

“Alikuwa akiwahamasisha uasi dhidi ya polisi na kutokata tamaa na kuwaeleza hata kama Sheikh Rogo na Sheikh Ibrahim wameuawa, basi wao bado wako wengi, watalipiza kisasi,” alisema Balozi, akinukuu maneno yaliyokuwa yakitolewa na Sheikh Juma.

Balozi Jecha alisema, Ubalozi wa Tanzania unaendelea kutafuta taarifa za raia huyo wa Tanzania, ikiwa ni pamoja na kujua iwapo aliingia nchini, na kwa njia zipi.

“Inawezekana kabisa bila shaka aliingia kwa kutumia hati halali ya kusafiria, lakini pia hatuna uhakika iwapo aliingia kwa njia za panya au vipi, tutatoa taarifa,” alisema Balozi huyo.

Wakati balozi huyo mdogo akitoa kauli hiyo, Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai nchini (DCI), Robert Manumba, alipotafutwa kuzungumzia suala hilo, hakupatikana na taarifa zilizolifikia gazeti hili zilieleza kuwa yuko nje ya nchi.

Wakati hayo yakiendelea, imebainika kuwa bado kuna vurugu kwenye msikiti huo na tayari Baraza la Maimamu la mjini Mombasa limeufunga Msikiti wa Masjid Mussa, hadi pale suala la usalama litakapotengemaa.

Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani nchini humo, Aggrey Adoli, mwishoni mwa wiki iliyopita alitoa wito kwa kiongozi huyo kujitokeza mwenyewe ili kutoa maelezo ya kilichotokea msikitini hapo.

“Tunataka kuweka ubinadamu mbele kwa kumuomba kiongozi huyo wa kidini ajipeleke polisi kwa hiari na kutoa maelezo bila kutulazimisha kutumia njia nyingine kumkamata,” alisema.

Hata hivyo, kauli ya juzi ya Adoli ya kumtaka sheikh huyo Mtanzania ajitokeze mwenyewe polisi inatofautiana na ile aliyoitoa Jumamosi kwa kusema kuwa kikosi cha kupambana na ugaidi kilimkamata mhubiri huyo na kuondoka naye mara baada ya kujitokeza nje ya msikiti huo.

Sheikh Juma anaelezwa kukubalika na idadi kubwa ya Waislamu mjini Mombasa, ambapo wafuasi wake waliamua kupambana na polisi muda mfupi mara baada ya swala ya Ijumaa.

Watu watano walikamatwa kufuatia purukushani hizo na walitarajiwa kufikishwa mahakamani jana.

CCM KWISHA KWISHA KABISA KIFO CHA MENDE MIGUU JUU 2015 !!!




UPEPO wa mabadiliko ya kisiasa unaovuma kuelekea kambi ya upinzani, sasa unaonekana kuwaamsha viongozi wa vyama hivyo baada ya kutolewa kwa taarifa kuwa wanafikiria kusimamisha mgombea mmoja wa urais kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Taarifa zilizolifikia gazeti hili kabla ya kuthibitishwa na mmoja wa viongozi hao, zilieleza kuwa hatua ya vyama hivyo imekuja baada ya ushirika wao waliouunda kupinga upungufu uliokuwemo kwenye Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kuzaa matunda.

Pamoja na hilo, inaelezwa kuwa maamuzi hayo magumu ya wapinzani yametiwa chachu na kauli aliyoitoa Rais Jakaya Kikwete ya hivi karibuni ya kukitabiria anguko Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika uchaguzi wa mwaka 2015 au ule wa 2020, kutokana na kile alichodai kuwa viongozi wa chama hicho kuendekeza rushwa.

Mmoja wa viongozi wanaounda ushirika huo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia alithibitisha taarifa hizo huku akisisitiza kuwa nia ya kufanya hivyo ni kuhakikisha wanaiondoa madarakani CCM mwaka 2015.

Kwa mujibu wa Mbatia, walichokifanya kwenye Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba si nguvu ya soda na badala yake wataendeleza hadi kwenye uchaguzi mkuu ujao.

Mbatia alisema kuwa uongozi wa vyama vya upinzani unatarajia kuungana na kumsimamisha mgombea mmoja, ili kuhakikisha wanaiondoa madarakani CCM.

Mbatia ambaye alikuwa akizungumza katika mahojiano maalumu na RAI Jumatano, alisema hatua hiyo pamoja na ushirika wao unalenga kudumisha amani na uzalendo kwa kuweka utaifa mbele.

Alisema umoja wanaoendelea kuuonyesha kwenye mchakato wa Katiba Mpya, ambao unalenga kuweka mbele maslahi ya Taifa ili kuhakikisha inapatikana Katiba bora yenye kushirikisha Watanzania wote, wataufanya pia kwenye chaguzi mbalimbali.

“Ili jambo lolote litokee lazima kuwepo na chanzo, mwanzo wetu wa ushirikiano ulioanza Septemba mwaka huu ndani ya ukumbi wa Bunge, tutauendeleza.

“Tupo kwenye maridhiano zaidi, hata muungano wetu wa Tanzania bara na Zanzibar si wa kisheria, viongozi wetu Nyerere na Mzee Karume walikaa na kuzungumza, hata sisi tunafanya hivyo, tunatakiwa kuzungumza kwa maslahi ya nchi,” alisisitiza Mbatia.

Alisema vyama vyao viliamua kuwa na ushirikiano wa pamoja kutokana na kubaini kwamba, bila umoja hakuna kitakachofanikiwa.

“Tumeshaanza kuzungumza kwa mapana juu ya ushirikiano wetu, ukweli ni kwamba kuna mwelekeo mzuri,” alisema.

Alisema hatua ya vyama kujadili kwa pamoja mchakato wa Katiba ni dalili njema za kuelekea kwenye mafanikio na ndio maana wanaona ipo haja ya kuuendeleza ushirika huo hadi kwenye chaguzi mbalimbali nchini.

“Tunapaswa kuvifanya vyama vyetu viwe vya maslahi mapana kwa taifa, ili visionekane vipo kwa ajili ya maslahi ya viongozi.

“Kwa kuwa tumeweka maslahi ya taifa mbele kwenye suala la Katiba, tumeona tuwe na mfumo ambao utalisaidia taifa, ndio maana hata tulipotoka Ikulu tumekubaliana kuwa Tanzania kwanza vyama baadaye, naamini kwa nia njema hata ule ushirikiano wetu utaendelea mbele zaidi kwa maslahi mapana ya taifa letu, tunategemea hivyo… tuna mategemeo mazuri, lazima tufikirie chanya,” alisema Mbatia.

Kauli ya Mbatia imeungwa mkono na Naibu Katibu Mkuu wa CUF Bara, Julius Mtatiro ambaye ameeleza kuwa chama chao hakina tatizo kwenye suala la kumsimamisha mgombea mmoja na wako tayari kwa sababu ushirikiano ni suala la msingi na lenye maana.

“Kulingana na upepo wa kisiasa ulivyo sasa, ni dhahiri tunahitaji kushirikiana ili kukiondoa chama tawala madarakani, kwa sababu mahali tulipo sasa ni pagumu.

“Tunachosubiri sasa ili kukamilisha muungano wetu ni tamko la pamoja kutoka kwa viongozi wa juu wa vyama vyote, lakini naamini nia ya kusimamisha mgombea mmoja itakubalika bila kupingwa,” alisema Mtatiro.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Habari kutoka Chadema, John Mnyika, alisema ushirikiano kwa sasa umejikita kwenye suala la kunusuru mchakato wa Katiba na kuwezesha nchi kupata Katiba bora.

Alisema ushirikiano katika masuala mengine ikiwamo pendekezo la kushirikiana katika uchaguzi, litatafakariwa kwa kuzingatia mafanikio katika ushirikiano kwenye suala la mchakato wa Katiba Mpya ambao tunaendelea nao kwa sasa.

“Huu ndio msimamo ambao naamini pia viongozi wote wanao.

“Kwa kuzingatia kauli zilizotolewa na wenyeviti wote watatu Septemba 15 mwaka huu kwenye mkutano na waandishi wa habari, wakati wa kutoa tamko la pamoja la ushirikiano,” alisema.

Hata hivyo, mchambuzi wa masuala ya siasa nchini, Dk. Benson Bana ameukosoa uamuzi huo kwa kudai kuwa hawawezi kuungana kwa sababu hawana kiwango cha kuing’oa CCM madarakani.

Dk. Bana aliweka wazi kwamba, hadhani kama vyama hivyo vitafaulu kuitoa CCM madarakani, kwa sababu havina mtaji wa kutosha wa wanachama.

Alieleza kuwa vyama vyote vitatu vinavyojiona vinaisumbua CCM, ambavyo ni CUF, Chadema na NCCR-Mageuzi, havijafanya utafiti wa kutosha kubaini mtaji wa wapiga kura walio nao.

Alisema Chadema ina nguvu ndogo Bara hasa kwenye maeneo ya mijini, CUF ina nguvu Zanzibar na NCCR-Mageuzi haina nguvu ya aina yoyote jambo linaloashiria udhaifu wa vyama hivyo, ambapo alivitaka kujipa muda wa kujipanga kabla ya kufikiria kuing’oa CCM.

Wenye mtazamo tofauti na huo wanasema kuwa endapo hatua hiyo ya vyama vya upinzani itafanikiwa, ni wazi itathibitisha kauli ya Mwenyekiti wa CCM kwamba chama hicho kijiandae kung’oka mwaka 2015 au 2020.

Hata hivyo bado kuna shaka juu ya maamuzi hayo ya vyama vya upinzani, kutokana na yale ambayo yamepata kushuhudiwa katika chaguzi nyingine zilizotangulia hususani zile za viti vya ubunge.

Imeshuhudiwa katika chaguzi kadhaa vyama hivyo vikisigana kufikia maamuzi ya kuachiana maeneo ya kusimamisha wagombea wenye nguvu.

Mwaka 2010 kwenye uchaguzi Mkuu, CUF kilikitaka Chadema kutosimamisha mgombea kwenye Jimbo la Tunduru kutokana chama chao kuwa na nguvu, hata hivyo wenzao walikataa.

Hali hiyo pia ilijitokeza kwenye Jimbo la Kiteto, Chadema iliitaka CUF kutosimamisha mgombea jambo ambalo halikutekelezwa.

Tuesday 29 October 2013

TEMBEZA UJUMBE HUU !!!


MAALIM SEIF AMPONDA MWENYEKITI WA ZEC!!!

Chama Cha Wananchi (CUF) kimesema kuwa  Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha, hana sifa za kushika wadhifa huo.

Akizungumza na wanachama na wapenzi wa CUF katika mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja vya Pwepweu Tumbe, Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, alisema Jecha ni mkereketwa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kwamba kwa mazingira hayo hataweza kutenda haki katika chaguzi.

Maalim Seif alidai kuwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, Jecha aliingia katika mchakato wa kugombea ubunge katika Jimbo la Kwamtipura kupitia CCM, lakini alishindwa.

Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar aliibua hoja hiyo baada ya kuwapo taarifa kuwa takwimu za wapiga kura wapya katika majimbo matano ya Unguja zimepotea kwenye kompyuta, na kudai kuwa huo ni mkakati maalum ulioandaliwa na CCM kwa kushirikiana na ZEC.

Ameyataja majimbo yanayodaiwa kupoteza takwimu zake za wapiga kura wapya kuwa ni Bumbwini, Donge, Kitope, Bububu na Mfenesini.

Maalim Seif alimtaka mwenyekiti huyo ajiuzulu wadhifa huo na kama akishindwa basi Rais wa Zanzibar achukue jukumu la kumfuta kazi.

“Kwa kweli huyu (Jecha) hana sifa kabisa za kuwa Mwenyekiti wa ZEC kwa sababu ni mkereketwa wa CCM aliyegombea nafasi ya ubunge katika uchaguzi mkuu wa 2010, hawezi kabisa kutenda haki katika uchaguzi,” alisema Maalim Seif na kuongeza:

“Kwa hivyo namuomba sana mwenyekiti huyu ajiuzulu, na kama akishindwa basi kwa heshima zote namuomba Rais Dokta Shein amwajibishe kwa kumfuta kazi.”
Jana mwenyekiti huyo alipotafutwa kuzungumzia madai hayo hakupatikana. Mkurugenzi wa ZEC, Salum Kassim, alisema kuwa Jecha alikuwa katika kikao.

Hata hivyo, mmoja wa maofisa waandamizi wa ZEC alisema waandishi wa habari wanaweza kuandika watakavyo.

Rais Shein alimteua Jecha kushika nafasi hiyo mwishoni mwa Aprili mwaka huu.
 

KINANA AZIMA MAPINDUZI UVCCM !!!

Mwenyekiti Sadifa acheza sakakasi kukwepa kung’olewa, amteua hasimu wake kisiasa, Makonda na wengine watatu kuongoza
Dodoma. Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana alilazimika kuzima mapinduzi yaliyokuwa yamepangwa kuwang’oa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Vijana ya chama hicho (UVCCM), Sadifa Juma Khamis na makamu wake, Mboni Muhita.
Jana Kinana akifungua mkutano wa Baraza Kuu la jumuiya hiyo, aliweka bayana kuwa mkutano huo haukuwa kwa ajili ya “kuibomoa UVCCM, bali kuijenga”, kauli ambayo inatajwa kuwa iliwavunja nguvu wajumbe waliokuwa wamepanga kuanzisha harakati za kuwatoa madarakani viongozi hao.
Habari zaidi kutoka Dodoma zilisema kauli ya Kinana iliongeza nguvu harakati za kujinasua za Sadifa ambaye usiku wa kuamkia jana, alikesha akifanya vikao vya kuwaomba radhi wenyeviti wa UVCCM wa mikoa na baadaye wajumbe wote wa Baraza Kuu.
“Hatua hiyo nadhani imemsaidia sana maana wenzake ndani ya umoja huo hawaridhiki na jinsi mambo yanavyokwenda, pamoja na uongozi wake. Wanaona kama hakidhi standards (viwango) zao,” kilisema chanzo chetu kutoka ndani ya mkutano huo.
Hii ni mara ya pili kwa Katibu Mkuu huyo kumwokoa Sadifa, kwani Septemba mwaka huu, alilazimika kuingilia kati mgogoro ambao uliibuka katika kikao cha Baraza Kuu la jumuiya hiyo Visiwani Zanzibar baada ya wajumbe kutaka kumwajibisha kwa madai kwamba alikiuka kanuni za uteuzi wa wakuu wa idara za UVCCM.
Pamoja na kauli elekezi ya Kinana, Sadifa ambaye pia ni Mbunge  wa Donge, Zanzibar alilazimika kucheza sarakasi zilizomwezesha kuzima mapinduzi yaliyokuwa yameandaliwa dhidi yake. Mwenyekiti huyo aliongoza kikao cha Baraza Kuu kwa saa tatu na kukamilisha ajenda zilizokuwa zimepangwa, ikiwa ni pamoja na kuwaidhinisha wakuu wapya wa idara za jumuiya hiyo,  kisha aliahirisha mkutano huo mara tu baada ya kuibuliwa kwa hoja ya kutaka kumjadili.
Habari zilizolifikia gazeti hili jana jioni zilisema, Mwenyekiti wa UVCCM, Mkoa wa Mbeya, Amani Kajuna ndiye aliyeibua hoja ya kutaka Sadifa ajadiliwe kutokana na kile alichosema kuwa kiongozi huyo ameifanya jumuiya hiyo kushindwa kutekeleza wajibu wake ipasavyo.
“Kama tunataka kusonga mbele katika jumuiya yetu, lazima tuhakikishe kwamba tunaisafisha nyumba yetu ili tukitoka hapa wote tuwe tunazungumza lugha moja. Kwa hiyo napendekeza mwenyekiti atoke nje ili tumjadili,” chanzo chetu kilimnukuu Kajuna.
Habari zaidi zilidai mapendekezo hayo ni kama yaliungwa mkono na baadhi ya wajumbe, akiwamo Mwenyekiti wa UVCCM wa Mkoa wa Dodoma, Henry Msunga ambaye alisimama na kusema: “Hiyo ni hoja ya msingi sana”.
Hata hivyo, wakati wajumbe wengine wengi wakiwa wameinua mikono yao juu wakitaka kuchangia pendekezo hilo, Sadifa alisimama na kuanza kuzungumza huku akiomba msamaha kwa upungufu wa kiuongozi unaojitokeza na katika hali isiyotarajiwa aliahirisha rasmi mkutano huo.


Kajuna na Msunga kwa nyakati tofauti jana, walilithibitishia gazeti hili kuwapo kwa matukio hayo, lakini walikataa kuyazungumzia kwa undani huku wakisema kuwa bado wana fursa katika vikao vijavyo kwa ajili ya kurekebisha mambo ndani ya jumuiya hiyo. “Mimi bado nina imani na jumuiya yetu, maana watendaji ambao tumewapitisha leo (jana) ninaamini watafanya kazi nzuri. Sisi viongozi wa mikoa tuko vizuri na tuna wanachama wengi, kwa hiyo jumuiya itaendelea kuwa imara,” alisema Kajuna.
Kwa upande wake, Msunga alisema: “Baada ya hoja kuibuliwa kweli mimi niliiona ni ya msingi sana, ila nimeridhika na maelezo kwamba mkutano ulikuwa na ajenda maalumu kwa hiyo ninachoamini ni kwamba fursa bado ipo, tutakapokutana tena tutakuwa na nafasi ya kurekebisha kasoro zinazojitokeza”.
Jitihada za kumtafuta Sadifa hazikufanikiwa jana, baada ya gazeti hili kuambiwa kuwa alikuwa kwenye kikao cha Kamati ya Utekelezaji ya jumuiya hiyo, kilichokutana jana usiku.
Chimbuko la mapinduzi
Mpango huo wa mapinduzi ulikuwa ni mwendelezo wa fukuto lililoanzia katika Mkutano Maalumu wa Baraza Kuu lililofanyika Zanzibar mapema Septemba mwaka huu, wakati wajumbe walipowakataa wakuu wa idara za UVCCM kwamba hawakuwa halali kutokana na uteuzi wao kutofuata taratibu na kanuni za jumuiya hiyo.
Mapema jana kabla ya kuzuka kwa hoja za kutaka kumjadili Sadifa, baraza hilo liliwapitisha wakuu wa idara wapya watatu akiwamo hasimu wa kisiasa wa mwenyekiti huyo wa UVCCM, Paul Makonda ambaye sasa ataongoza Idara ya Chipukizi na Uhamasishaji.
Makonda mara baada ya kushindwa katika Uchaguzi Mkuu wa jumuiya hiyo mwishoni mwa mwaka jana alipokuwa akiwania nafasi ya makamu mwenyekiti, aliteuliwa kuwa mjumbe wa Baraza Kuu lakini aliikataa nafasi hiyo.
Hatua hiyo ilimgharimu katika kikao cha Baraza Kuu la UVCCM, Februari mwaka huu, wakati alipokwenda Dodoma kwa mwaliko wa kuhudhuria kikao hicho, lakini baada ya kuchukua posho, alitimuliwa kwa maelezo kwamba aliwahi kukataa nafasi hiyo.
Taarifa ambazo gazeti hili lilizipata na kuthibitishwa na Katibu Mkuu wa UVCCM, Sixtus Mapunda zilisema wengine walioteuliwa na kuidhinishwa na Kikao cha Baraza Kuu ni Zainabu Katimba atakayeongoza Idara ya Oganaizesheni na Omari Suleiman ambaye amepewa Idara ya Fedha na Uchumi.
Sadifa ambaye pia ni Mbunge wa Donge aliwahi kulalamika juu ya kuwapo kwa kundi la vijana ambao wamekuwa wakimpiga vita sambamba na kuingilia utendaji wa kazi zake za kila siku kinyume cha katiba ya jumuiya hiyo.

Monday 28 October 2013

MCHUMBA ANASWA AKIJIUZA ,AZIMIA

Mchumba huyo wa mtu aliyejitambulisha kwa jina moja la Diva alitoa kali ya mwaka baada ya kuzimia ghafla huku akitokwa na mapovu kinywani baada ya kunaswa na OFM akijiuza.
Tukio hilo lilitokea wiki iliyopita maeneo ya Kimboka, Buguruni, Dar ambapo msichana huyo pamoja na ‘madadapoa’ wenzake walikuwa wakifanya biashara hiyo haramu bila kificho.
Mara baada ya kuona wenzake wakiwa mikononi mwa nguvu za dola katika kamatakamata ya polisi, mrembo huyo ambaye baadaye alijitambulisha kama mchumba wa mtu, alianguka ghafla na kuzimia kiasi cha kuzua hofu miongoni mwa machangu wenzake walioangua kilio wakidhani mwenzao amekata ringi (kufa).
Baada ya muda msichana huyo alirejewa na fahamu akiwa mikononi mwa polisi na kuanza kuangua kilio akiomba asikamatwe kwa kuwa yeye ni mchumba wa mtu na atakuwa kwenye wakati mgumu kama mchumba’ke atajua anajiuza.
“Naomba msinikamate. Mimi ni mchumba wa mtu afande. Mtaniweka kwenye wakati mgumu kama akijua nilikuwa nikijiuza. Jamani nitamkosa mchumba wangu Luka,” alisema mrembo huyo huku akiomba maji ya kunywa.
Hata hivyo, kilio chake hakikuwazuia ‘OFM’ kufanya kazi yake ndani ya Kituo cha Polisi Buguruni, Dar  ambapo watuhumiwa hao wanasubiri kupandishwa kizimbani kwa ajili ya taratibu za kisheria.

Sunday 27 October 2013

MAGEUZI KATIBA MPYA !!!


RASIMU ya awali ya Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo imekwishajadiliwa katika Mabaraza ya Katiba na sasa inafanyiwa uchambuzi na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, inafanyiwa mabadiliko kadhaa ya msingi huku mfumo wa Serikali Tatu ukiendelea kubaki kama ilivyopendekezwa, Raia Mwema limeelezwa.

Kati ya mambo ya msingi ambayo yataingizwa katika awamu ya pili ya rasimu ya Katiba Mpya ikakayowasilishwa kwa Rais na kisha katika Bunge la Katiba mara baada ya kukamilika ni pamoja na mipaka kati ya Tanganyika na Zanzibar, kuongozwa kwa mambo ya Muungano kutoka saba yaliyopendekezwa awali hadi 10, kinga dhidi ya mashitaka ya Rais, majimbo ya ubunge kwa Bunge la Muungano, ulinzi na usalama pamoja na vyama vya siasa kuweza kufukuza wabunge walioshinda kwa ridhaa ya vyama hivyo.

Mipaka ya Tanganyika na Zanzibar
Mipaka ya Tanganyika na Zanzibar ni lazima iwekwe ndani ya Katiba ili kila mamlaka ya nchi washirika iendeshe shughuli zake bila kuingiliana. Uchimbaji wa mafuta au uvuvi wa samaki, Tanganyika ijue iishie wapi na Zanzibar iishie wapi.

Kwa sasa katika rasimu ya Katiba Mpya, sura ya kwanza inayozungumzia mipaka, alama, lugha, utamaduni na tunu za taifa, ibara yake ya pili inaeleza kuhusu eneo la Jamhuri ya Muungano kuwa ni eneo lote la Tanzania Bara ikijumuisha sehemu yake ya bahari na eneo lote la Zanzibar ikijumuisha sehemu yake ya bahari.

Mambo ya Muungano kutoka saba hadi 10

Kwa sasa, katika rasimu ya kwanza ya Katiba mpya, mambo ya Muungano yanatajwa kuwa saba ambayo ni mosi, Katiba na mamlaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; pili, ulinzi na usalama wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; tatu, uraia na uhamiaji; nne, sarafu na benki kuu; tano, mambo ya nje; sita, usajili wa vyama vya siasa na saba; ushuru wa bidhaa na mapato yasiyo ya kodi yatokanayo na mambo ya Muungano.

Katika mambo hayo saba, yatanatarajiwa kuongezwa matatu kwa mujibu wa maoni yaliyotolewa wakati wa Mabaraza ya Katiba. Yanayoweza kuongezwa ni Haki za Binadamu, Tume Huru ya Uchaguzi, Maadili na Miiko ya Uongozi.

Kinga dhidi ya mashitaka ya Rais
Rasimu ya kwanza ya Katiba mpya iliyojadiliwa katika Mabaraza ya Katiba ilipendekeza katika Ibara ya 83(1) na (2) kuhusu kinga dhidi ya mashitaka ya Rais. Katika ibara hiyo ya 83 (1) inaeleza; Wakati Rais akiwa madarakani, hatashitakiwa wala mtu yeyote hataendesha mashtaka ya aina yoyote dhidi yake mahakamani kwa ajili ya kosa lolote la jinai.

Ibara ya 83(2) inaeleza; wakati Rais ameshika madaraka kwa mujibu wa Katiba hii, haitaruhusiwa kufungua mahakamani shauri la madai kuhusu jambo lolote alilolitenda au alilokosa kulitenda yeye binafsi kama raia ama kabla au baada ya kushika madaraka ya Rais, ila tu kama angalau siku thelathini kabla ya shauri kufunguliwa mahakamani, Rais atapewa au ametumiwa taarifa ya madai kwa maandishi kwa kufuata utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge, na taarifa hiyo ikiwa inatoa maelekezo kuhusu chanzo cha shauri hilo, kiini cha madai yenyewe, jina lake na anwani ya mahali anapoishi huyo mdai na jambo hasa analodai.

83 (3) inaeleza; isipokuwa kama ataacha kushika madaraka ya Rais kutokana na kura ya kutokuwa na imani na Rais, haitakuwa halali kwa mtu kumshitaki au kufungua mahakamani shauri lolote la jinai au la madai dhidi ya mtu aliyekuwa anashika madaraka ya Rais baada ya kuacha madaraka hayo kutokana na jambo alilofanya wakati alipokuwa bado anashika madaraka ya Rais.

Katika eneo hili kuhusu kinga dhidi ya mashitaka ya Rais, maoni mengi ambayo yanapewa nafasi kubwa kuwekwa katika rasimu ijayo ya Katiba mpya itakayowasilishwa katika Bunge la Katiba ni kutaka kuwapo na mwanya wa kumshitaki Rais baada ya kuondoka madarakani, hasa kwa makosa ambayo atakuwa amefanya yasiyohusiana na madaraka yake ya urais.

“Huwezi kuwa na kinga ya jumla katika kumshitaki Rais ambaye amekwishaondoka madarakani, tunaweza kuwa na kinga ya kutomshitaki kwa mambo ambayo ameyafanya kama Rais na lakini lazima kuwe na nafasi ya kumshitaki kwa mambo ambayo ameyafanya akiwa madarakani ambayo si sehemu ya majukumu ya Rais. Kwa mfano, ikitokea Rais amehusishwa na matukio ya hovyo kama ubakaji. Jiulize, ubakaji ni kazi za Rais…kama siyo kwa nini asishtakiwe baada ya kuondoka madarakani?” kilieleza chanzo chetu cha habari.

Majimbo ya Bunge la Muungano utata

Kwa kuzingatia maoni ya wadau wengi wa Mabaraza ya Katiba, kumekuwa na hali ya kupaki njia panda katika Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ambayo katika rasimu yake ya awali ilipendekeza katika Ibara ya 105 (2) kuhusu aina za wabunge ambao ni (a) waliochaguliwa kuwakilisha majimbo ya uchaguzi (b) wabunge watano watakaoteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye sifa za kuchaguliwa kuwa waunge kuwakilisha watu wenye ulemavu kwa kuzingatia uwiano wa Washirika wa Muungano.

Wednesday 23 October 2013

,WIZARA YA ELIMU ZANZIBAR HAIJASHIRIKISHWA KUYATOWA MASOMO YA DINI NA KIARABU !!!


Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar imesema Masomo ya Dini,Kiarabu na Masomo mengine hajafutwa na yataendelea kusomeshwa na kufanyiwa Mitihani katika ngazi zote kama ilivyokuwa hapo awali.

Aidha imesema Wizara hiyo haijakubaliana na Waraka wa Elimu kutoka Tanzania Bara wa kuyafanya Masomo hayo kuwa ya hiari na hivyo yasichangie asilimia yoyote katika ufaulu wa Mtahiniwa.

Naibu katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu Zanzibar Abdallah Mzee ameyasema hayo leo alipokuwa akizungumza na Waandishi wa habari kwa lengo la kukanusha Taarifa zilizotolewa na baadhi ya Vyombo vya habari zilizodai kuwa Wizara hiyo imeondoa Mtaala wa Masomo ya Dini na Kiarabu kwenye Mitihani ya Taifa.

Amefahamisha kuwa Watendaji kutoka Wizara ya Elimu Tanzania Bara walikutana na Wenzao kutoka Zanzibar kwa lengo la kujadili Waraka wa Elimu waliokuja nao uliokuwa unataka kufanyike mambo mapya.

Mzee amebainisha kuwa katika Waraka huo Wenzao kutoka Bara walipendekeza kuwa Masomo ya Dini ya Kiislam, Dini ya Kikristo, Lugha ya Kiarabu, Kifaransa, Komputa, Mziki yawe ya Hiari kwa Mwanafunzi kuyasoma lakini pia yasisaidie ufaulu wowote katika viwango vya Madaraja ya Ufaulu.

“Waraka ulipendekeza Masomo hayo yakiwemo Dini na Kiarabu kuwa Optional na wala yasisaidie chochote katika kupandisha au kushusha Division ya Mtahiniwa” Alifafanua Mzee.

Aidha ilipendekezwa kuwa Utaratibu huo mpya uanzwe kufanyiwa kazi kwa Wanafunzi watakaoingia Kidato cha Kwanza mwakani ili ifikapo mwaka 2017 wanafunzi hao wautumie katika kidato cha nne.

Hata hivyo Naibu Katibu Mkuu huyo alisema kuwa Watendaji wa Zanzibar waliupinga utaratibu huo kwa vile haukidhi matakwa ya Zanzibar.

“Watendaji wetu Waliupinga Waraka huo kwani hautufai na unatofautiana sana na Sisi kulingana na hoja zetu tulizotoa,lakini pia walikubali kuurudisha ili usiweze kufanyiwa kazi ” alisema Naibu Katibu Mkuu huyo.

Alisema kwa Zanzibar, Wizara ya Elimu inatoa Mchepuo wa Masomo ya Lugha katika Skuli tofauti ikiwemo Sekondari ya Kiponda hivyo itakuwa vigumu kufuata utaratibu huo.

Kuhusu Somo la Dini Mzee amesema Somo hilo kwa Zanzibar ni muhimu sana na nimiongoni mwa masomo yenye Walimu Wazuri wa ngazi za Stashahada hadi Udaktari-PHD ambapo ufundishwaji wake huanzia darasa la kwanza hadi Chuo Kikuu hivyo kubadili utaratibu isingewezekana.

Aidha amefahamisha kuwa katika dunia ya sasa Somo kama Komputa ni muhimu sana hivyo kulifanya halina ulazima ni kujirudisha nyuma kimaendeleo.

Amesema licha ya mahusiano mazuri yaliyopo baina ya Wizara kwa upande wa Zanzibar na Bara lakini Wao hawakushirikishwa katika Uanzishwaji wa Waraka huo.

Katika hali ya kuliweka sawa jambo hilo Mawaziri wa Wizara hizo Ali Juma Shamhuna na Mwenzake wa Bara Shukuru Kawambwa wanatarajia kukutana kesho kulijadili jambo hilo.

Monday 21 October 2013

INAUMA WEWE ,LAKINI BASI MUNGU ATALIPA ,SOMA HAPA ,

Waziri wa Kilimo wa Jamhuri ZA Muungano wa Tanzania yupo UK kwa mualiko wa Serikali ya UK, Lakini Kilimo sio suala la Muungano na katika msafara wake hakuna Mwakilishi wa Serikali ya Zanzibar ambayo imeunda hiyo Jamhuri.
Wenzetu wanasema hizi kero wanazisikiliza na kuzifanyia kazi, [Mashuduu]. Katika ziara hi kama msaaada wa wataalamu ama wa mali wote huishia Tanganyika chini ya koti la jina la Tanzania. Na hili ni moja tu ya mifano Elfu.
Mh Christopher Chiza atafanya mkutano hapo kwenye Ubalozi, hivyo kila mwenye nafasi ya kutaka kumsikiliza na pia kumuuliza Masuali anakaribishwa tarehe 23 mwezi huu. Saa kumi na Moja jioni majira ya UK
Ningependa mkajitokeza kwa wingi kama mnayo nafasi.

Wednesday 16 October 2013

UAMSHO 'HATUJABADILISHA KAULI ZANZIAR KWANZA !!!

Na Waandishi Wetu. MIEZI 12 baada ya kukamatwa na kufunguliwa kesi inayohusu mashtaka ya uchochezi na kushawishi fujo, masheikh na viongozi wa Uamsho hawajabadilika.
Viongozi hao walio chini ya mwamvuli wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislam (JUMIKI) wanaendelea na msimamo wao wa kutaka kuona Zanzibar inarejesha mamlaka yake kamili ya kujiendesha kama dola huru.
“Msimamo wangu mimi na wenzangu ni uleule. Ingawa tuna mwaka mmoja sasa tuko gerezani, tungali na msimamo wetu uleule wa kupigania Zanzibar. Hii ni nchi yetu na tuna haki ya kuitetea kikamilifu,“ anasema Sheikh Azzan Khalid Hamdan, mmoja wa masheikh hao.
Sheikh Azzan ambaye ni Naibu Amir wa Uamsho, ametoa kauli hiyo katika mahojiano maalum na Zanzibar Daima Online, yaliyofanyika nyumbani kwake Mfenesini, nje kidogo ya mji wa Zanzibar, siku moja kabla ya kiongozi huyo kuondoka nchini kuelekea India kwa matibabu.
Anasema hakuna sababu ya kuonekana wao eti wameondoka kwenye malengo ya kuanzishwa kwa jumuiya hiyo kwa kuwa hata taasisi ya dini kama hiyo yao, inao wajibu wa kushughulikia maslahi ya wananchi.
“Si sawa jumuiya yetu kuchukuliwa kuwa imekiuka sheria za kuanzishwa kwake. Jumuiya inapaswa kuwa karibu na kujihusisha hasa na mas’ala yanayohusu haki ya wananchi,“ alisema Sheikh Azzan akiwa anajibu hoja inayotolewa mara kwa mara ndani ya Serikali na katika mazungumzo ya watu wa kawaida kwamba jumuiya ya Uamsho imevunja sheria kwa kujihusisha na harakati za kupigania mustakbali wa Zanzibar.
Anasema yeye na wenzake wanaamini kuwa hawajavunja sheria yoyote kwa sababu kama ni hivyo, Serikali ingekwishaifuta jumuiya hiyo ambayo ilisajiliwa kwa mujibu wa sheria za Zanzibar mwaka 2003.
“Wanajua kwamba hatujavunja sheria yoyote mpaka sasa. Shughuli yetu tumezifanya kwa mujibu wa sheria. Hawa watu wa Serikali wanajua kuwa tungekuwa hatuna uhalali, wangekwishatufuta kwenye usajili. Hawajafika hapo kwa sababu tupo kwenye misingi za sheria.
“Hao wanatusingizia kuhusika katika matukio ya uhalifu na matukio ya kutia watu tindikali, wanajua wanatuonea. Wanajua hatuhusiki. Nasi kwa kinywa kipana kabisa, tunasema hatuhusiki kwa namna yoyote na matukio haya ya kuchafua watu, ya kujeruhi watu kwa risasi au kwa kuwamwagia tindikali. Mara zote na kila tunapoyasikia, tunasikitika na kuwalaani kwa nguvu wale wanaoyatenda,’’ anasema.
Katika hoja kwamba watu wengi ndani ya nchi Zanzibar, ndani ya Tanzania na ulimwenguni wanainasibisha jumuiya yao na makundi mabaya ya kigaidi kama Al Shabaab, Al Qa’eda na Boko Haram, anasema ni bahati nzuri hakuna mwenye ushahidi wa mnasaba huo.
“Kuna watu wana chuki tu na sisi. Kwa sababu ya chuki zao dhidi yetu, wanasema watakavyo juu yetu. Wanatuhusisha na uhalifu unaofanywa wakati sisi tuko gerezani. Inawezekana wanaofanya wanajulikana lakini wanalindwa kwa sababu wanazozijua hao wanaowatuma. Ni chuki yao tu hawana ushahidi hata chembe wa kuhusika kwetu.
“Hata hiyo kesi waliyotufungulia, ni chuki tu waliyonayo baadhi ya viongozi. Na ndo maana nasema mimi na wenzangu tuna ujasiri wa kusema watoe ushahidi wa sisi kuhusika na matukio hayo… Hii kesi ina mwaka mzima sasa haijasikilizwa. Ni kwa sababu hawana ushahidi,’’ anasema.
Sheikh Azzan na wenzake tisa wamekuwa kwenye gereza la Kiinua Miguu, lililopo Kilimani, mjini Zanzibar wakiendelea kusota huko wakati kesi walizofunguliwa hazijapata kusikilizwa.
Wengine ni Masheikh Mselem bin Ali Mselem, Farid Hadi Ahmed, Suleiman Juma Suleiman, Mussa Juma Mussa, Abdalla Said Madawa, Fikirini Khamis Fikirini, Gharib Said, Khamis Suleiman Ali na Hassan Bakari.
Walikamatwa Oktoba 16 katika maeneo tafauti ya mjini Zanzibar, na siku tatu baadaye ndipo walipelekwa mahakamani kwa mashtaka ya kula njama ya kutenda jinai. Baadaye mashtaka yalibadilishwa na kuwa ya kushawishi watu kufanya fujo – uchochezi.
Wanatuhumiwa kuvunja Sheria ya Usalama wa Taifa ya mwaka 1968 ambayo inasimamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
Kwa sasa wanakabiliwa na kesi mbili ambazo mashtaka yake yanafanana, moja ikiwepo Mahakama ya Wilaya iliyopo Mwanakwerekwe na nyingine mbele ya Mahakama Kuu, Vuga.
Sheikh Farid ndiye kiongozi wa Maimamu wa Zanzibar, ambaye kutoweka kwake kwa siku tatu ambako masheikh wenzake walikulalamikia ndiko chimbuko la kukakamatwa kwao.
Sheikh Farid alitoweka katika mazingira ya kutatanisha akiwa eneo la Mombasa Kwa Bakathir usiku wa siku hiyo, na akaibuka siku tatu baadaye majira yaleyale ya usiku na palepale alipokuwa amechukuliwa na watu ambao hajawahi kuwataja kwa kudai hawafahamu.
Jeshi la Polisi lilimwita na kumhoji atoe ushahidi wa madai yake kuwa alitekwa na watu wa Serikali. Alipofika kituoni Mwembemadema, yalipo makao makuu ya Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, alishikiliwa na halafu wakakamatwa masheikh wengine tisa walio ndani mpaka sasa.
Dhamana yao imezuiliwa na Mahakama kutokana na Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar (DPP), Ibrahim Mzee, kusema wasitolewe kwa dhamana.
Ila Sheikh Azzan, yeye yuko nje kwa dhamana iliyotolewa na Mahakama Kuu wiki iliyopita ili kumwezesha kusafiri nje ya nchi kwa ajili ya matibabu.
Ombi lake ambalo lilisikilizwa na kuamuliwa na Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu, lilikuwa ni jitihada za mwisho za mawakili wake na masheikh wenzake baada ya kupata maradhi ya vijiwe kwenye figo ambayo yamemzidi gerezani kiasi cha kuanguka na kuzimia mara tano, mara mbili ikiwa ndani ya gereza.
Kabla ya hapo, alikuwa amelazwa Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja, mjini Zanzibar. Mbele ya Jaji Makungu, mawakili waliwasilisha maelezo ya madaktari yaliyomthibitisha kuwa ni mgonjwa na hakuna hospitali ndani ya nchi inayoweza kumtibu isipokuwa kupelekwa nchini India.
Sheikh Azzan anatarajia kusafiri wiki hii kwenda India kwa matibabu ambayo anajilipia kwani serikali imesema haina uwezo wa kumpeleka haraka hivyo kwa kuwa wapo wagonjwa waliomtangulia ambao wangali wanasubiri kupatikana fedha ili wapelekwe nje ya nchi kutibiwa.
Akizungumzia maisha ya gerezani, alisema ni ya unyonge mkubwa, yasiyopendeza na yanayosikitisha.
“Angalau siku hizi kuna afadhali kidogo. Zile siku 42 za kwanza tulipoingia tu gerezani zilikuwa siku mbaya na ngumu sana. Tukiishi katika upweke na udhalilishaji mkubwa. Tulipofika tu tulinyolewa ndevu. Tukawa tunakaa mbali na watu. Kwa wiki nzima tulikuwa hatukutanishwi. Tumetengwa.
“Tukiishi katika vyumba vidogo na vya kiza. Afya zetu zimeathirika sana kwa kila mmoja na hali yake. Siku hizi angalau tunapata taarifa za yanayotokea huku nje, tafauti na siku zile tulipoingia,’’ anasema.
Alipoulizwa kama anajua kwa nini wako gerezani, labda anajua wana kesi gani, Sheikh Azzan alisema yeye hajui anashtakiwa kwa sababu gani. Anaona hawana kesi yoyote ila wamefungwa kwa sababu viongozi wametaka wafungwe.
Sheikh Azzan anasema kwa kuendelea kukaa gerezani, huduma mbalimbali za kusaidia watu dhalili walizokuwa wakizitoa zimezorota. Shughuli zao za kimaisha pia zimekufa na familia zao zimepata pigo kubwa.
“Tulikuwa tunahudumia watoto yatima zaidi ya 1,000 kupitia jumuiya yetu ya Uamsho. Hatujui wanapata vipi huduma sasa. Wengine tukiwasomesha, hatujui maendeleo yao. Baadhi wako nje ya Zanzibar, hatujui hatma zao. Wakati ule ilikuwa dhima kwetu lakini kwa sababu tumetiwa gerezani, dhima yote imemuangukia Rais Dk. Shein. Yeye anajua kwa nini sisi tuko gerezani, yeye ndo Rais anajua sababu.
“Dk. Shein tunamwambia aliapa, tena kwa kushika Mas’hafu kuwa atakuwa mwadilifu. Sasa tungependa aoneshe uadilifu, atende uadilifu. Sisi tunaendelea kukaa gerezani kwa sababu viongozi wa Serikali wameamua tu tukae ndani, hakuna ushahidi wa kesi yetu. Hawana ushahidi, wangeuleta na kesi ikaendelea. Kwa hivyo dhima anayo Rais,’’ anasema.
Sheikh Azzan anasema walichokuwa wanakipigania ni lazima kiendelee kupiganiwa na Wazanzibari kwa sababu anasema walianzisha kampeni kwa madhumuni ya kuhangaikia maslahi ya Wazanzibari ambayo yamekuwa yakidhoofishwa na watu wabaya.