Sunday 27 October 2013

MAGEUZI KATIBA MPYA !!!


RASIMU ya awali ya Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo imekwishajadiliwa katika Mabaraza ya Katiba na sasa inafanyiwa uchambuzi na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, inafanyiwa mabadiliko kadhaa ya msingi huku mfumo wa Serikali Tatu ukiendelea kubaki kama ilivyopendekezwa, Raia Mwema limeelezwa.

Kati ya mambo ya msingi ambayo yataingizwa katika awamu ya pili ya rasimu ya Katiba Mpya ikakayowasilishwa kwa Rais na kisha katika Bunge la Katiba mara baada ya kukamilika ni pamoja na mipaka kati ya Tanganyika na Zanzibar, kuongozwa kwa mambo ya Muungano kutoka saba yaliyopendekezwa awali hadi 10, kinga dhidi ya mashitaka ya Rais, majimbo ya ubunge kwa Bunge la Muungano, ulinzi na usalama pamoja na vyama vya siasa kuweza kufukuza wabunge walioshinda kwa ridhaa ya vyama hivyo.

Mipaka ya Tanganyika na Zanzibar
Mipaka ya Tanganyika na Zanzibar ni lazima iwekwe ndani ya Katiba ili kila mamlaka ya nchi washirika iendeshe shughuli zake bila kuingiliana. Uchimbaji wa mafuta au uvuvi wa samaki, Tanganyika ijue iishie wapi na Zanzibar iishie wapi.

Kwa sasa katika rasimu ya Katiba Mpya, sura ya kwanza inayozungumzia mipaka, alama, lugha, utamaduni na tunu za taifa, ibara yake ya pili inaeleza kuhusu eneo la Jamhuri ya Muungano kuwa ni eneo lote la Tanzania Bara ikijumuisha sehemu yake ya bahari na eneo lote la Zanzibar ikijumuisha sehemu yake ya bahari.

Mambo ya Muungano kutoka saba hadi 10

Kwa sasa, katika rasimu ya kwanza ya Katiba mpya, mambo ya Muungano yanatajwa kuwa saba ambayo ni mosi, Katiba na mamlaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; pili, ulinzi na usalama wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; tatu, uraia na uhamiaji; nne, sarafu na benki kuu; tano, mambo ya nje; sita, usajili wa vyama vya siasa na saba; ushuru wa bidhaa na mapato yasiyo ya kodi yatokanayo na mambo ya Muungano.

Katika mambo hayo saba, yatanatarajiwa kuongezwa matatu kwa mujibu wa maoni yaliyotolewa wakati wa Mabaraza ya Katiba. Yanayoweza kuongezwa ni Haki za Binadamu, Tume Huru ya Uchaguzi, Maadili na Miiko ya Uongozi.

Kinga dhidi ya mashitaka ya Rais
Rasimu ya kwanza ya Katiba mpya iliyojadiliwa katika Mabaraza ya Katiba ilipendekeza katika Ibara ya 83(1) na (2) kuhusu kinga dhidi ya mashitaka ya Rais. Katika ibara hiyo ya 83 (1) inaeleza; Wakati Rais akiwa madarakani, hatashitakiwa wala mtu yeyote hataendesha mashtaka ya aina yoyote dhidi yake mahakamani kwa ajili ya kosa lolote la jinai.

Ibara ya 83(2) inaeleza; wakati Rais ameshika madaraka kwa mujibu wa Katiba hii, haitaruhusiwa kufungua mahakamani shauri la madai kuhusu jambo lolote alilolitenda au alilokosa kulitenda yeye binafsi kama raia ama kabla au baada ya kushika madaraka ya Rais, ila tu kama angalau siku thelathini kabla ya shauri kufunguliwa mahakamani, Rais atapewa au ametumiwa taarifa ya madai kwa maandishi kwa kufuata utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge, na taarifa hiyo ikiwa inatoa maelekezo kuhusu chanzo cha shauri hilo, kiini cha madai yenyewe, jina lake na anwani ya mahali anapoishi huyo mdai na jambo hasa analodai.

83 (3) inaeleza; isipokuwa kama ataacha kushika madaraka ya Rais kutokana na kura ya kutokuwa na imani na Rais, haitakuwa halali kwa mtu kumshitaki au kufungua mahakamani shauri lolote la jinai au la madai dhidi ya mtu aliyekuwa anashika madaraka ya Rais baada ya kuacha madaraka hayo kutokana na jambo alilofanya wakati alipokuwa bado anashika madaraka ya Rais.

Katika eneo hili kuhusu kinga dhidi ya mashitaka ya Rais, maoni mengi ambayo yanapewa nafasi kubwa kuwekwa katika rasimu ijayo ya Katiba mpya itakayowasilishwa katika Bunge la Katiba ni kutaka kuwapo na mwanya wa kumshitaki Rais baada ya kuondoka madarakani, hasa kwa makosa ambayo atakuwa amefanya yasiyohusiana na madaraka yake ya urais.

“Huwezi kuwa na kinga ya jumla katika kumshitaki Rais ambaye amekwishaondoka madarakani, tunaweza kuwa na kinga ya kutomshitaki kwa mambo ambayo ameyafanya kama Rais na lakini lazima kuwe na nafasi ya kumshitaki kwa mambo ambayo ameyafanya akiwa madarakani ambayo si sehemu ya majukumu ya Rais. Kwa mfano, ikitokea Rais amehusishwa na matukio ya hovyo kama ubakaji. Jiulize, ubakaji ni kazi za Rais…kama siyo kwa nini asishtakiwe baada ya kuondoka madarakani?” kilieleza chanzo chetu cha habari.

Majimbo ya Bunge la Muungano utata

Kwa kuzingatia maoni ya wadau wengi wa Mabaraza ya Katiba, kumekuwa na hali ya kupaki njia panda katika Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ambayo katika rasimu yake ya awali ilipendekeza katika Ibara ya 105 (2) kuhusu aina za wabunge ambao ni (a) waliochaguliwa kuwakilisha majimbo ya uchaguzi (b) wabunge watano watakaoteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye sifa za kuchaguliwa kuwa waunge kuwakilisha watu wenye ulemavu kwa kuzingatia uwiano wa Washirika wa Muungano.

1 comment: